Mkoani Kigoma,Serikali ya Wadau kuendelea kuboresha huduma zaAfya
Serikali kwa kushirikiana na wadau wameendelea kupiga hatua muhimu kuelekea kufikia malengo endelevu ya mwaka 2030 ya kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi kufikia vifo 70 kwa vizazi hai laki moja na vifo vya watoto wachanga kufikia vifo 12 katika vizazi hai elfu moja. Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Balozi Simon Sirro, aliyewakilishwa na Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt. Rashid Chuachua kwenye uzinduzi wa mradi wa Mjamzito na Mtoto Salama utakaotekelezwa na Shirika la Thamini Uhai, ukilenga kuchangia katika juhudi za serikali za kupunguza vifo vya uzazi na watoto wachanga. Amesema hatua hizo ni pamoja na kuboresha na kuimarisha miundombinu pamoja na vifaa tiba kwenye sekta ya afya, na kwamba juhudi zinazofanywa na wadau kama vile Shirika la Thamini Uhai ni muhimu katika kufikia malengo hayo. Mwakilishi kutoka Wizara ya Afya Joachim Masunga, amesema kupitia mradi wa Mjamzito na Mtoto Salama, utaleta tija kubwa kwenye jitihada za kupambana na vifo vitokanavyo na uzazi. ...