Adaiwa kuiba kichanga ili kulinda ndoa

JESHI la polisi mkoani Rukwa linamshikilia Magreth Juma (34), mkazi wa mtaa wa Chanji Manispaa ya Sumbawanga kwa tuhuma za wizi wa mtoto mchanga wa siku mbili.
Mtuhumiwa huyo, alikamatwa Oktoba 22 asubuhi nyumbani kwake maeneo ya Chanji akiwa na mtoto huyo wa kike, ikiwa ni muda mfupi tangu aibiwe kutoka kwa mama mzazi huko Bangwe umbali wa takribani kilomita 15.
Inadaiwa kuwa, awali taarifa zilifikishwa kituo cha polisi Sumbawanga majira ya alfajiri na mama wa mtoto huyo, Magreth Benisia (28), kuwa mtoto wake mchanga amepotea katika mazingira ya kutatanisha akiwa nyumbani kwake, ndipo polisi walianza msako mkali kwa kushirikiana na raia wema na muda mfupi baadaye waliweza kumkamata mtuhumiwa huyo akiwa na mtoto nyumbani kwake.
Baada ya kukamatwa, katika maelezo yake ilibainika kuwa mama wa mtoto aliyeibiwa na ndugu wa mtuhumiwa waliwahi kuishi nyumba moja ya kupanga, hivyo kusababisha mtuhumiwa kumfahamu vizuri mama huyo wa mtoto na hivyo kuwa rahisi kwake kutenda kosa hilo.
Uchunguzi ulibainisha kuwa, mtuhumiwa huyo ambaye ni mama wa watoto watatu aliozaa na mume wake mwingine mbali na anayeishi naye sasa, ameweza kuishi na mume wake wa sasa kwa zaidi ya miaka miwili bila kupata mtoto mwingine, hali iliyoanza kuhatarisha ndoa yake, kwani mwanaume huyo amekuwa akitaka kupata mtoto na ndio maana mama huyo aliamua kuiba mtoto katika harakati za kuilinda ndoa yake.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao