Profesa Shivji: Migogoro ya ardhi ni adui wa maendeleo ya wananchi

Kwa muda mrefu, Serikali imekuwa ikianzisha mipango, sera, miradi na mikakati mbalimbali yenye lengo kuinua uchumi nchini.
Licha ya mipango hiyo kuwapo, bado kumekuwa na ugumu katika kufikia mafanikio yaliyotarajiwa kutokana na sababu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuwa na mipango na mikakati mingi kwa wakati mmoja pamoja, hali kadhalika uwapo wa migogoro ya ardhi katika vijijini vingi nchini.
Wakati kukiwa na ugumu huo, inaelezwa kuwa asilimia 70 ya Watanzania wanajishughulisha na kilimo, lakini wengi wanashindwa kufikia malengo kutokana na migogoro ya ardhi.
Baadhi ya mipango ya Serikali ya kuinua uchumi ni pamoja na Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kuondoa Umasikini (Mkukuta), Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara Tanzania (Mkurabita), Mkakati wa Maendeleo ya Sekta ya Kilimo (ASDS). Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo (ASDP), Kilimo Kwanza, Uendelezaji Kilimo Ukanda wa Kusini Tanzania (SAGCOT), Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambao ulianza mwaka 2011-2016 na Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Profesa Issa Shivji ni mmoja kati ya waanzilishi wa taasisi ya utafiti na utetezi wa haki za ardhi inayoitwa HakiArdhi. Taasisi hiyo ilianzishwa mwaka 1994 kwa ajili ya kuhakikisha kuwa wananchi wanatumia ardhi kwa ajili ya maendeleo kwa kuwa ardhi ni gurudumu la maendeleo.
Akizungumzia maadhimisho ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa taasisi hiyo, Profesa Shivji anasema: “Huwezi kuzungumza mfumo wa umiliki ardhi nje ya mwelekeo na mfumo wa nchi. Jiulize, unataka nani au kundi gani katika nchi liwe gurudumu la maendeleo.”
Profesa Shivji, ambaye alikuwa mwenyekiti wa Tume ya Ardhi iliyoundwa mwaka 1990 ya Rais Ali Hassan Mwinyi kwa ajili ya kuangalia matatizo na migogoro ya ardhi nchini na baadaye kutoa mapendekezo.
Tume hiyo ilipendekeza kuwa gurudumu la maendeleo liwe wazalishaji wadogo, hasa wa vijijini na hivyo lazima wazalishaji hao washirikishwe katika suala zima la ugawaji wa ardhi.
“Kuna mjadala mkubwa tu na upande mmoja unasema ni wawekezaji. Sasa kama umeamua wawekezaji ndio watakuwa watu wa kutuletea maendeleo, lazima upore ardhi kwa wanakijiji na kuwapatia wawekezaji,” anasema.
“Kama unakubali kwamba mchango wa wawekezaji hautakuwa mstari wa mbele na wazalishaji wadogo ndiyo watapewa kipaumbele, lazima uondoe hofu juu ya ardhi kwa wazalishaji hao.”
Anasema msingi mkuu wa kuanzisha Taasisi ya HakiArdhi mwaka 1994 ni baada ya kuona mapendekezo makuu ya tume hiyo kutozingatiwa na Serikali.
“Inatakiwa iwe hivi. Serikali ikitaka ardhi kwa manufaa ya wananchi, lazima iwashirikishe wananchi husika na waelezwe na kukubali,” anasema.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao