Ukawa waanza kugawana Majimbo

Moshi. Baada ya kumalizika kwa Bunge la Katiba, hasira za Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) dhidi ya CCM zimehamia kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2015, safari hii ukiunda kamati maalumu kutafuta namna ya kumsimamisha mgombea mmoja wa urais na kuachiana majimbo.
Mwenyekiti mwenza wa Ukawa, James Mbatia ametoa maelezo hayo alipokuwa akizugumza na gazeti hili katika mahojiano maalumu hivi karibuni.
Mbatia ambaye pia ni Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, alisema tayari kamati zimeundwa na zinaendelea na kazi ya kuratibu mpango huo mahususi, unaolenga kuiondoa CCM madarakani.
“Lengo letu ni kuhakikisha Ukawa ina nguvu ya kushika dola katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 na katika mpango huo, vyama vitaachiana majimbo na viti vya udiwani kulingana na nguvu ya chama katika sehemu husika,” alisema.
Ukawa; umoja ulioanzishwa Februari mwaka huu ukiwa ni kikundi shinikizi katika mchakato wa Katiba katika siku za mwanzo za Bunge Maalumu la Katiba, unaundwa na vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema, CUF na NLD.
Mbatia alisema anaamini kwa mkakati huo uliopangwa na Ukawa, CCM itakuwa na wakati mgumu katika uchaguzi mkuu ujao.
“Sasa hivi ziko kamati zinaaendelea na maandalizi ya namna ya kushirikiana katika uchaguzi mkuu ujao na nataka nikuhakikishie siku za Serikali ya CCM zinahesabika,” alisema Mbatia na kuongeza:
“Kamati hii inatafiti ni namna gani bora ya kuachiana madiwani, wabunge na rais ili tusimamishe mgombea mmoja katika kila eneo na tutakubaliana nani asimame wapi.”
Mbatia alisema uchaguzi mkuu ujao utamalizika kwa wabunge wengi wa upinzani kuingia bungeni na iwapo mambo yatakwenda kama walivyopanga, CCM kinaweza kuwa chama cha upinzani.
“Kwa sasa wagombea kutoka Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD ni ruksa kutangaza nia, lakini kamati yetu itasema nani miongoni mwao ateuliwe kupeperusha bendera ya Ukawa,” alisema.
Mbatia aliwahakikishia Watanzania kuwa ushirikiano wa vyama hivyo si nguvu ya soda na kusisitiza kuwa wanaofikiri ushirikiano huo utavunjika kuelekea Uchaguzi Mkuu 2015 ni ndoto za mchana.
“Kwanza tumekwishaunda Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, tuko pamoja na lengo letu tunakuwa na ushirikiano ambao umeonekana tangu Bunge la Jamhuri, Bunge la Katiba na sasa hivi Ukawa.”

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao