Jeshi la Ukraine na wawakilishi wa waasi wanaotaka kujitenga wamebadilishana wafungwa kadhaa gizani katika eneo la mapigano jana Jumamosi(21.02.2015) na kuanzisha mchakato wa kuleta amani mashariki mwa Ukraine.

Wanajeshi 139 na waasi 52 walibadilishwa, kwa mujibu wa afisa wa wanaotaka kujitenga ambaye ameshuhudia hatua hiyo ya mabadilishano ya wafungwa katika eneo ambalo halidhibitiwi na upande wowote karibu na kijiji cha Zholobok, kiasi ya kilometa 20 magharibi ya mji unaoshikiliwa na waasi wa Luhansk.

Basi lililojaa wanajeshi wa Ukraine wakiwa katika sare za jeshi liliwasafirisha wanajeshi hao mapema siku hiyo kutoka jimbo ambalo ni ngome kuu ya waasi wa Donestk hadi katika eneo la vijijini kiasi ya kilometa 140 kaskazini mashariki , kabla ya kujiunga na makundi mengine ya wafungwa wenzao.


Baada ya kuwasili katika eneo katika mji wa Zholobok , wanajeshi hao walipangwa katika mistari na kusikiliza hotuba iliyotolewa na wawakilishi wa waasi, ambao wamewaamuru watu hao kuondoka katika eneo hilo linalodaiwa na wapiganaji wanaotaka kujitenga katika majimbo ya Donetsk na Luhansk.
Wanajeshi, baadhi yao wakitembea kwa kutumia magongo, wakati mmoja akiwa amebebwa katika machela, walitembea kwa karibu kilometa tatu hadi katika eneo la makutano.Rais wa Ukraine Petro Poroshenko ameandika katika ukurasa wake wa Twitter kwamba amearifiwa kuwa mchakato mzima ulianzia katika idara ya usalama wa taifa.
Haifahamiki watu wangapi wanashikiliwa
Msemaji wake , Svyatoslav Tsegolko, baadaye amesema mwanajeshi mmoja zaidi wa Ukraine mfungwa ataachiwa huru katika siku zijazo.
Makubaliano ya amani yaliyotiwa saini wiki iliyopita mjini Minsk yameelekeza katika mabadilishano ya wafungwa wote katika mzozo huo.
 Haifahamiki ni watu wangapi wanashikiliwa kwa jumla katika pande zote , licha ya kwamba wapiganaji wanaotaka kujitenga katika mji wa Donetsk wamesema Ukraine inawashikilia kiasi ya waasi 580 kama wafungwa.
Waasi wamesema idadi kubwa ya wanajeshi wa Ukraine walioachiliwa siku ya Jumamosi wamekamatwa wakati wa mapigano ya hivi karibuni kwa ajili ya mji muhimu wa Debaltseve, ambao umekamatwa na wapiganaji wanaotaka kujitenga wiki iliyopita.
Jamhuri iliyojitangaza ya watu wa Donestk imeeleza katika taarifa kwamba wengi wa watu waliokabidhiwa kwa maafisa wa Ukraine walikuwa ni raia.
Lakini "wachache kiasi ya asilimia 50 ya wale waliohusika katika mabadilishano kutoka kwa jamhuri ya watu wa Donestk walikuwa wafungwa wanajeshi," taarifa hiyo imesema.
Taarifa ya waasi imedokeza kile ilichosema ni waangalizi katika mabadilishano hayo wakisema wengi wa wafungwa walioachiliwa huru na serikali ya Ukraine wana ishara za kutendewa vibaya.
"Baadhi ya wafungwa hawakuweza kutembea wenyewe.
Wakati huo huo , wafungwa wote wanajeshi waliokabidhiwa kwa wawakilishi wa Ukraine walikuwa katika hali nzuri," taarifa hiyo imesema.


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao