Tanzania tuitakayo na njia ya kuifikia


Kwa Wenyeviti wa vyama vyote vya Siasa hapa Nchini

Ccm, Chadema, Nccr Mageuzi, Cuf Udp, na vinginevyo



Ndugu zangu, na viongozi wangu


Yah: Tanzania tuitakayo na njia ya kuifikia
Ninajisikia vyema kuwaletea waraka huu nikiwa na matumaini kuwa mtausoma kwa makini na kuupa uzito unaostahili na ikibidi kuufanyia kazi kama kila mmoja wenu atakavyoona na/au kwa pamoja kama ninavyopendekeza bila kujali umetoka wapi kwa sababu mimi ni raia wa kawaida asiye na jina linalojulikana, Tanzania.

1.0        Utangulizi
Sasa hivi Tanzania iko katika mchakato wa kuandika Katiba mpya. Japo hatujajua Watanzania watapata katiba ya namna gani lakini kuna uwezekano mkubwa kwamba tutapata katiba mpya. Matumaini ya wengi ni kuwa Katiba hiyo itaweza kutoa mwelekeo wa kutatua matatizo na changamoto ambazo zimejitokeza hivi karibuni na pia kuelekeza Taifa hili liweje siku za usoni.

2.0        Mazingira tuliyomo.
2.1        Tunaweza kuyasoma mazingira tuliyomo kwa namna mbali mbali. Mimi ningependa kujadili mazingira tuliyomo kwa kuzingatia jambo hili: Ujirani na mataifa mengine na hali ya siasa katika eneo letu hili sasa na mbele tuendako: Nafasi ya Tanzania katika ushawishi wa kisiasa, kiuchumi hata kiusalama katika eneo letu.

2.2        Kwa muda toka tumepata uhuru Tanzania imekuwa na mchango mkubwa wa kuyasaidia mataifa yaliyotuzunguka kujipatia uhuru wao. Nchi zote zimepata uhuru angalau wa bendera. Ukiziangalia nchi zinazotuzunguka licha ya kwamba nasi bado tuna matatizo ya demokrasia yetu, lakini naweza kusema kwa ujasiri kuwa Tanzania ina utulivu wa kisiasa kuliko majirani zetu. Tumeweza kubadilishana viongozi wa Juu bila mikwaruzo mikubwa, angalau hatujawahi kulazimika kusuluhishwa kutoka nje. Si kwamba tunaridhika na kila kitu lakini angalau si kama majirani zetu.

2.3        Tukiyapima mataifa yanayotuzunguka unaona nchi nyingi zina migogoro au zina uwezekano mkubwa wa kuibuka migogoro na hata kupigana. Nchi zinazotuzunguka zina vikundi vilivyo na silaha na wengine hawataki hata kusuluhishwa, kwa hiyo kuna uwezekano wa kuendelea na migogoro. Katika mazingira kama haya eneo linahitaji nchi ambayo majirani wanaweza kuiheshimu, kuikimbilia kuomba msaada wa kutatua matatizo yake, lakini hata kuiogopa kidogo (Regional Power).
Ukiuliza mtu yeyote atakwambia ni Tanzania yenye uwezo wa kuwa hivyo. Na mimi nawaza hivyo.

2.4        Lakini nikiiangalia Tanzania naona licha ya kuwa ndilo taifa pekee linaloweza kukimbiliwa na majirani zake lakini sioni kama lina uwezo kamili wa kufanya hivyo.

2.5        Nawaza kuwa ili taifa liweze kuwa kamili na tayari kufanya hivyo lazima liwe na mambo makubwa manne:
  1. Liwe na Demokrasia nzuri.
  2. Liwe na Uchumi imara,
  3. Liwe na Jeshi imara na
  4. Liwe na Usalama wa Taifa imara.

2.6        Mimi siamini kuwa haya manne tuko imara kiasi cha kuwaangalia majirani wakatuheshimu. Kumekuwa na migogoro na mijadala na majirani zetu wa Malawi na Rwanda. Nimeshiriki kujadili habari hizi kupitia mitandao ya jamii hasa Wanabidii. Ninaamini kama balaa lingeingia tukaingia vitani na mmoja wa majirani hawa, Tanzania tungeshinda vita hiyo. Lakini ukweli tungeingia vitani. Ninaposema kuwa na jeshi imara nina maana kuwa na jeshi ambalo nchi jirani zinaogopa kupigana nalo hivyo hawawezi kuwa wa kwanza kutuchokoza kwa kuwa wanaogopa.

2.6.1     Demokrasia:
Hata kama Tanzania inayo demokrasia lakini malalamiko na mahusiano ya wanasiasa wetu ni ya kimaslahi zaidi kuliko kujenga nchi. Ukiangalia utakuta watanzania hatuna kitu kinachotuunganisha. Hatuna lengo la kiuchumi ambalo kila Chama cha siasa kinajieleza kitalitimizaje. Sikukuu za kitaifa hazituunganishi. Nadra kuwakuta viongozi wetu wa vyama vya siasa mmekutana katika siku hizi au siku nyingine mmeitana kushauriana juu ya jambo fulani la kitaifa. Katika ziara za kikazi viongozi wetu wa serikali hukosi alama za vyama vya siasa au matamshi ya kukejeliana. Hii sio maana hasa ya siasa tunayoitamani. Tunahitaji kujenga demokrasia ya kweli ambayo tutapingana katika mambo ya msingi na kukubaliana katika mambo ya msingi. Ninaamini tunaweza kuwa na demokrasia ambayo tunatofautiana mbinu ya kutimiza malengo yetu.
Ninakumbuka wakati taifa la Israel lilipotuma askari wake kuwakomboa wenzao waliokuwa wametekwa na kuletwa Entebe Uganda, waziri mkuu wa Israel alimtaarifu kiongozi wa upinzani kwanza. Walibishana kwanza na baadaye wakakubaliana na ndiye aliyekuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari baada ya operation hiyo.
Tanzania kwa mazingira tuliyo nayo tunahitaji siasa hizo zaidi. Sasa tumegawanyika kiitikadi kiasi badala ya siasa kutuunganisha inatutenganisha. Hii inaweza kulipeleka taifa pabaya achilia mbali kulizuia kwenda mbele.

2.6.2     Uchumi:
Tanzania ina nafasi nzuri za kujenga uchumi wake na wananchi wake wakaondokana na umaskini. Nitataja maeneo ninayoyaona kuwa yanaweza kuliendeleza taifa hili kila moja likiwa peke yake:
a)         Bandari, na reli. Tanzania ina eneo kubwa la bahari. Ninaamini kama Tanzania ikijenga bandari za kisasa tatu tu Tanga, Dar Es Salaam na Mtwara; Ikaimarisha reli za kati na Tazara inaweza kuwahudumia nchi jirani zisizo na mlango wa bahari, na kukusanya mapato ya kutosha kuendesha nchi hii bila misaada wala mikopo mikubwa kutoka ndani na nje. Tunahitaji kuweka misingi ndani katiba zetu na mifumo yetu ya uongozi zitakaotusaidia hata kuchagua rafiki. Kuna nchi zina bandari nzuri na tunaweza ama kuiga kwao au kwenda kujifunza kwao na tukajenga zetu.

b)         Madini na gesi asilia: Wote tutakumbuka kuwa nchi kama Libya wakati wa Ghadafi wananchi wake walineemeka na raslimali mafuta. Kama tukiweka kwenye katiba yetu namna nzuri ya kuwanufaisha watanzania tunaweza kujikuta hatulazimiki kutoza wananchi wetu kodi kubwa kwa sababu ya kiburi cha utajili huo wa madini na gesi.

c)         Ardhi yenye rutuba: Tanzania ni nchi iliyoneemeka kuwa na ardhi inayoweza kulimika. Kama Tanzania ikipunguza eneo linalolimwa na mkulima mdogo mdogo, na eneo litakalolimwa likalimwa kisasa (intensive farming), mazao yatakayolimwa yatatosheleza mahitaji ya ndani na kuuza ziada nje na eneo kubwa likabaki kwa ajili ya mifugo na kupanda misitu hivyo kulinda mazingira. Niliwahi kufanya utafiti na kugundua kuwa kilimo bora cha migomba ekari moja inatosheleza mahitaji ya chakula kwa familia kumi na moja.
Maana yake kama kilimo kikisimamiwa; badala ya 80% ya watanzania kuwa ‘wakulima’ watapungua hadi 20% na hao watalisha nchi nzima na kuuza ziada nje bila kulazimika kuwaita wakulima wakubwa kutoka nje. Faida yake ni kuwa:
i)   Eneo dogo tutajilisha na kulisha jirani zetu.
ii)  Maeneo yaliyobaki tutatenga kwa ajili ya mifugo
iii)  Na maeneo mengine yatabaki kustawisha mazingira kwa kuoteza misitu na kuweka kwa kilimo cha baadaye.

d)         Utalii: Tuna vyanzo vingi vivutio vya utalii. Maziwa, Mbuga nakadhalika. Tukiwekeza katika maeneo hayo Tanzania itajenga uchumi wake na wananchi wake na hivyo kupunguza kutegemea misaada. Kilimo na utalii vinawezekana bila misaada kutoka nje.

2.6.3     Jeshi na usalama wa Taifa:
Kama tukiwa na demokrasia ya kweli na uchumi mzuri Tutalazimika kujenga vyombo hivi viwili na wala hakuna nchi inayoweza kutushtukia. Tutakuwa na uwezo na sababu. Uimara wa jeshi unaweza kutatua migogoro ya jirani zetu si kwa kuwalazimisha lakini kwa kuwashauri na pengine kuwabana watende haki kwa raia wake. Nikiangalia mazingira ya nchi ya Syria; kama si uwezo wa kijeshi wa nchi za magharibi huenda Syria isingesalimisha silaha za sumu. Tanzania tuliisaidia nchi ya Comoro kuukomesha uasi uliojitokeza. Msaada uliotolewa Comoro kutoka Tanzania hatuwezi kuutoa Kenya mambo yakibadilika. Tuna nafasi ya kuwa na uchumi imara kuliko majirani zetu na hivyo kujenga ulinzi wetu kwa manifaa yetu na jirani zetu.

3.0        Mchakato:
Tanzania inahitaji kuandaa vision yake katika kujenga taifa kama nilivyolieleza (au hata la namna nyingine). Na baada ya kuiandaa vision hiyo tunahitaji kuwa na mfumo wa kuiendesha kupitia vyama vingi. Ni vizuri kujifunza kwa mataifa mengine; yaliyoendelea na yanayoendelea. Kitu kimoja nafikiri ni muhimu ni kuwa lazima vision hiyo iandaliwe na watanzania wote bila kujali tofauti zao kiimani, kieneo (hasa eneo la Muungano) na kiitikadi pia. Na hasa kuweka mpango ambao unaweka mipaka ya itikadi. Tuwe na tunu za kitaifa na namna ya kuziendesha. Mathalan tukisema sikukuu za kitaifa watu wote wanajumuika hatutegemei kuwakuta wenzetu wa chama fulani hawapo kwa vyovyote vile.

Ili kujenga mfumo huo tunahitaji kuwa na kipindi cha mpito. Kipindi ambacho tutakitumia kufanya maamuzi kama waTanzania na hata kupanga mipaka hiyo ya itikadi zetu.
Ili kufikia hapo tunahitaji mambo mawili:

1= Kuwa na kipindi cha uongozi wa Mpito ambamo licha ya vyama vyetu kuendelea kufanya kazi zake kama kawaida lakini kipindi hicho kisigubikwe na mkanganyiko wa kiitikadi kama sasa.
2=Kipindi hicho kuongozwa na Rais ambaye tumemkubali kama watanzania kukiongoza. Rais huyo aonekane kuwa na sifa zifuatazo:
  • Muumini wa dini lakini asiye na ‘udini’.
  • Mzanzibari (au Mtanganyika) asiye na Uzanzibari (au Utanganyika), bali yeye Uzanzibari wake una maana kama utanganyika kwa manufaa ya Muungano.
  • Mwanachama wa chama cha siasa asiyetawaliwa na Itikadi za chama chake, bali anautanguliza utanzania mbele.

Kiongozi huyo aliongoze Taifa kwa kipindi cha miaka mitano na moja kati ya kazi zake ni kuwaunganisha watanzania na kuwaandaa kufanyika uchaguzi wa vyama vingi katika mfumo wa kuheshimu malengo ya taifa. Alisaidie Taifa katika kipindi hicho kujenga misingi ya UTAIFA kwa vitendo.

4.0        Manufaa ya mpango huu
Mpango huu una manufaa makubwa sana.
1          Kwanza hebu tukubali kuwa tumetingishika kidogo. Taifa limeshuhudia mambo fulani yaliyojitokeza na kuonyesha kugawanyika.
2          Pili hebu tukubali kuwa kila kundi linaona linaweza kutatua matatizo tuliyo nayo. Na kila kundi linataka kufanya hivyo kulishinda kundi jingine. Hii ni nzuri kama ni jambo la kawaida. Lakini kunapokuwa hata na amani inatishiwa, ni ngumu kufanikisha. Kwa hiyo kuwa na serikali inayoungwa na wote ambamo mafanikio yake hayatamnufaisha mmoja wapo, ni mpango mzuri.

3          Lakini manufaa mengine ni kule kuamua wenyewe kuwa na uongozi wa Mpito. Karibuni Zimbabwe ilikuwa na uongozi wa pamoja. Kenya vile vile. Maamuzi yalitoka nje ya nchi hizo. Kwa hiyo sisi kuona hivyo na tukasema tunapumuzisha itikadi zetu katika uongozi wa miaka mitano ili kukamilisha mambo fulani mataifa yote yataishangaa na kuipongeza Tanzania. Licha ya kuwa sifa nyingi zinaweza kuiendea serikali iliyopo madarakani lakini vyama vyote kuunga mkono mpango huu katika uchaguzi ni sifa kwa taifa zima.
4          Manufaa ya nne baada ya hapo Tanzania itakuwa imara na sifa zake zilizolegea baada ya rais wa awamu ya kwanza zitarudi pale pale.
5          Manufaa mengine ni kupata mwanzo mzuri wa uendeshaji wa nchi baada ya katiba mpya ambomo moja kati ya mabadiliko yanayotarajiwa ni Nchi kuwa na Serikali tatu.

5.0        Mapendekezo:
Naomba kujitetea kuwa mimi si mwanasiasa na si mzoefu wa miundo ya serikali. Lakini nina mapendekezo yanayoweza kurekebishwa katika mchakato kama inavyoweza kuonekana inafaa.
1)       Rais.
Napendekeza mtu ninayemuwazia kuongoza serikali hii kuwa ni Salim Ahmed Salim
Akikubaliwa ataunda serikali kwa uhuru kamili kwa mujibu wa katiba iliyopo/itakayokuwepo na hatalazimika kuchagua mawaziri wake kutoka chama chake bali atakavyoona inafaa

2)       Bunge
Bunge litachaguliwa kutokana na wagombea wa vyama vya siasa kwa mujibu wa katiba iliyoko/itakayokuwapo, isipokuwa Chama Cha mapinduzi hakitatumia Jina la Salim kuwanadi wabunge wake.

3          Ili kuhakikisha hili linafaya kazi wakati wa kampeni ya Rais kutakuwa na wawakilishi wa vyama vyenu nilivyoviandikia na vingine vinavyounga mpango huu/mgombea huyu mkono. Vyama ambavyo havitakubaliana na mpango huu vitakuwa vimesimamisha wagombea urais wake. Ikitokea vyama vyote vikauunga mkono basi kura ya Rais itakuwa ya ndiyo na hapano.

Napendekeza kwenu kuwa kama mpango huu utakubaliwa basi Rais Kikwete aitishe kikao cha faragha kuujadili nami nikaribishwe katika kikao hicho ili kujieleza kama kuna mahala sijaeleweka lakini na kuweka mawazo yanayoweza kuwa yamebaki bila kujitokeza ndani ya waraka huu.

Ninapendekeza pia kuwa Mpango huu ukikubalika MIMI ndiye niwakilishe pendekezo hili Kwa Salim (au mtu mwingine anayeweza kuonekana anafaa). Sababu ni njema ili kumuonyesha kuwa wazo lilikotoka mahala fulani.na hkama hii itawakilisha maslahi ya vyama vyote vinavyoshiriki.

Natanguliza shukrani zangu za dhati kwa uaminifu wenu kwa taifa hili si kwa kuyaheshimu mawazo haya ninayoyatoa bali na kazi nyingine mnazoonekana kuzifanya katika mfumo huu wa vyama vingi.

Ndimi mtanzania mwenzenu

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao