USHAWISHI: Lowassa amponza profesa wa Udom

Dar es Salaam. Profesa wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom), Peter Kopoka amebanwa na uongozi wa chuo hicho kutokana na kushiriki maandamano ya kwenda nyumbani kwa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kumshawishi achukue fomu ya kugombea urais.

Profesa huyo akiwa na wahadhiri pamoja na watu wengine walioelezwa kuwa ni wanafunzi wa vyuo vikuu mkoani Dodoma walifanya maandamano hayo Machi 22, mwaka huu.
Kutokana na tukio hilo, uongozi wa Udom umemtaka ajieleze kwa nini ameshiriki harakati hizo za kisiasa huku akijua kuwa ni mtumishi wa umma anayepaswa kuwahudumia watu wenye itikadi tofauti.

Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Idris Kikula alisema kwa kuwa jambo hilo lilionekana kukiwakilisha chuo katika masuala ya siasa, uongozi ulilazimika kumhoji mhadhiri huyo.

“Ametuandikia barua ya kujieleza na kubainisha kuwa alikwenda yeye binafsi na siyo kama mwakilishi wa chuo. Lakini mambo haya ni magumu sana kutofautisha. Mimi kwa mfano, siwezi kwenda sehemu halafu nikasema sikwenda kama mkuu wa chuo kwa sababu siwezi kutofautisha hilo. Lakini tumechukua maelezo yake na tumeyahifadhi,” alisema Profesa Kikula.

Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa akiwasalimia wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali vya mjini Dodoma na waendesha bodaboda walioandamana kwenda nyumbani kwake mjini humo jana kwa ajili ya kumshawishi achukue fomu ya kuwania Urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu. Picha na Anthony Siame
Kuhusu wanafunzi wanaodaiwa kushiriki harakati hizo kutoka chuoni hapo, alisema hakuna wanachoweza kufanya kwa sababu mbili kubwa. Kwanza, ni vigumu kuwatambua waliofanya hivyo na pili walifanya hivyo nje ya chuo, jambo linalowezekana.

“Maandamano hayo yalifanyika mtaani. Huko walikuwa wanavunja sheria za nchi, kama hayakufuata sheria, Jeshi la Polisi ndilo lenye mamlaka ya kudhibiti au kuruhusu jambo kama hilo kufanyika,” alisema. Alipoulizwa kuhusu suala hilo, Profesa Kopoka alikiri kuandika barua hiyo na kueleza kuwa alichokifanya ni kutekeleza haki yake ya uraia ya ushiriki katika utawala wa haki na demokrasia nchini.

“Nimefanya hivyo. Nilikwenda kutokana na imani yangu kutokana na vile ninavyomfahamu Lowassa. Sikuwa peke yangu. Ni kama ilivyoripotiwa, walikuwapo pia wahadhiri kutoka vyuo vikuu vya Mtakatifu Yohana (St. John) na Mipango,” alisema Profesa Kopoka.
Alisema pamoja na kufanya hivyo, suala hilo halijaathiri utendaji wake wala mkataba wake wa ajira.
Mfululizo wa kukanusha

Siku nne baada ya maandamano hayo, viongozi wa Serikali za wanafunzi kutoka vyuo vikuu mbalimbali walijitokeza na kukanusha habari hiyo kwa maelezo kuwa waliofanya hivyo hawakuwa wanafunzi na wala suala hilo halikupata baraka kutoka vyuoni.
Katika taarifa ya pamoja ya marais wa serikali za vyuo vikuu hivyo vilivyomo mkoani humo iliyosomwa na Rais wa St. John, Daniel Daniel imepinga kushiriki kwao na kubainisha kuwa waliofanya hivyo ni watu wa mtaani.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao