Ikulu: JK hajazuia kampeni, ni sheria

Dar es Salaam. Ikulu imesema kuwa Rais Jakaya Kikwete hajazuia kufanyika kwa kampeni kuhusu Kura ya Maoni isipokuwa Sheria ya Kura ya Maoni ndiyo inayozuia  kufanyika kwa kampeni hizo kwa sasa.
Mkurugenzi wa Mawasiliano, Ikulu, Salvatory Rweyemamu alisema hayo Dar es Salaam jana na kuongeza kuwa sheria hiyo inaelekeza kampeni kufanywa ndani ya siku 60 kabla ya kufanyika ya kupiga kura ya maoni.
“Kimsingi Rais hajakataza kampeni, Sheria ya Kura ya Maoni ndiyo inayokataza, lakini kinachofanyika ni kutoa elimu kama inavyofanya Serikali, hiyo inaruhusiwa...Serikali haifanyi kampeni, nasisitiza,” alisema.
Rweyemamu alisema hayo baada ya Rais Kikwete kuwahutubia Wazee wa Mkoa wa Dodoma, Jumapili iliyopita.
Alipoulizwa kuwa Ikulu inafanya kazi ya asasi za kiraia zilizoainishwa kwa mujibu wa sheria kufanya kampeni za kuelimisha umma kuhusu Kura ya Maoni, Rweyemamu  alisema Ikulu inatoa somo la uraia lakini si kupiga kampeni.
Alipotakiwa kueleza kama ni elimu, kwanini inawataka Watanzania kupiga kura ya ndiyo, Rweyemamu alisema: “Tunatoa civic education (elimu ya uraia) na hiyo ya  kusema wapige kura ya ndiyo, haikatazwi kwani wapi kuna sheria inayokataza Serikali kutoa elimu?”
Hata hivyo, Rweyemamu alisema kuwa Serikali ndiyo yenye mchakato wa Katiba hivyo haikatazwi kupigia kampeni.
“Utakaaje kimya wakati watu wanapiga kampeni huko? Sisi tumeingia mtaani baada ya wengine kufanya hivyo, japokuwa kuna utaratibu wake,” alisema.
Kauli ya JK Dodoma
“Ninaomba Watanzania wenzangu tuzingatie mamlaka ya Sheria ya Kura ya Maoni ambayo imeelekeza vizuri lini kura ya maoni itapigwa na lini kampeni zitafanyika na lini wadau watatoa elimu, naomba tuwe na subira. Tukizingatia sheria hii hakuna  ugomvi,”alisema Rais Kikwete.
Alisema ni vyema kusubiri hadi tume itakapotoa maelekezo ya utekelezaji huo kwa kuwa muda wa kampeni na utoaji elimu kwa umma bado.
Rais Kikwete alisema sheria ipo na imepangwa siku maalumu za kufanya hivyo.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao