Malima ahimiza uwekezaji

SERIKALI imesema kuwa uchumi wa nchi hauwezi kukua bila ya kuwepo na uwekezaji wenye tija kwa taifa na jamii kwa ujumla.

Rai hiyo ilitolewa jijini Dar es Salaam jana na Naibu Waziri wa Fedha, Adam Malima wakati akifungua semina ya kujadili matokeo ya Afrika katika uchumi, iliyoandaliwa na wizara hiyo kwa udhamini wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).

Alisema uwekezaji ndio unaosaidia kukuza uchumi wa taifa lolote duniani, hivyo bila ya kuwa na sekta binafsi zitakazoweza kuwekeza katika nyanja mbalimbali za maendeleo uchumi hautaweza kukua.

“Unajua kuwa ukuaji mzuri wa uchumi unasukumwa na sekta binafsi na kama tunataka kuwa na maendeleo hapa kwetu ni lazima tuangalie ni njia gani zitumike ili uchumi unaokuwa uwanufaishe wananchi wote na si wachache. Ndio maana hawa wenzetu wa AfDB wametupatia fedha ili zitumike katika maeneo sita waliopendekeza wao ambayo wanadhani yanaweza kukuza zaidi uchumi wetu,” alisema.

Malima aliyataja maeneo hayo sita kuwa ni uwongozi bora, uwajibikaji, uwezo wa kutumia mifumo ya kiteknolojia, uwezo wa kitaasisi kuwasilisha huduma ipasavyo kwa jamii, matokeo ya kibajeti pamoja na uwezo wa wanahabari kutoa habari sahihi kwa jamii.

Alisema uchumi wa Tanzania utaendelea kukua siku hadi siku kutokana na serikali kutoa fursa kwa wawekezaji kuwekeza nchini na kuongeza kuwa ripoti ya uchumi iliyotolewa na AfDB inaonyesha kuwa Tanzania inaendelea kufanya vizuri kwenye sekta ya uchumi.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao