Serikali yaridhia ujenzi wa hoteli

Arusha
. Hatimaye Serikali imetoa idhini ya ujenzi wa hoteli ya kitalii katika eneo jirani na Kingo za Kreta ya Ngorongoro, eneo ambalo awali lilitangazwa kupigwa marufuku kufanyika kwa ujenzi wa aina yoyote.
Akizungumza jana jijini hapa, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyarandu alisema mchakato wa ujenzi wa hoteli hiyo itakayomilikiwa na Kampuni ya Kibo Palace itakayojengwa katika eneo la Alaiyanai, ulianza miaka tisa iliyopita.
“Mradi huu ulianza miaka zaidi ya tisa iliyopita na ulipitishwa, kwa kuwa Serikali ni moja, lazima tuheshimu makubaliano lakini kwa miradi mingine mipya ambayo watu wengi wameomba kujenga pembeni mwa kreta hatutaruhusu,” alisema Nyarandu.
Alisema uamuzi wa kupinga ujenzi wa hoteli za kitalii kuzunguka kreta upo pale pale na kamwe hautabadilika.
Hata hivyo, alisema kutokana na Serikali kuridhia ujenzi huo, Hifadhi ya Ngorongoro ipo hatarini kuondolewa kuwa moja ya maeneo ya urithi wa dunia na Shirika la Uhifadhi la Umoja wa Mataifa (Unesco).
Akizungumzia ujenzi huo, Katibu wa Baraza la Wafugaji wa Ngorongoro, ambalo limekuwa likipinga ujenzi wowote kuzunguka kreta, James Moringe alisema bado hawajapata taarifa rasmi za kujengwa kwa hoteli hiyo.
Alisema taarifa walizonazo zinaeleza kuwa, mkataba wa ujenzi ulishasainiwa miaka tisa iliyopita na ujenzi huo ukasitishwa.
Moringe alisema hoteli hiyo ilitakiwa kujengwa katika eneo la Nainokanoka ambako baadaye ilibainika kuwa eneo hilo ni la mazalia ya faru. Ujenzi huo unapingwa kwa madai kuwa unachangia uharibifu wa mazingira ya kreta.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao