IPTL yazamisha mawaziri, AG, wabunge

Dodoma.
 Bunge limehitimisha mjadala wa Kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow kwa kupitisha maazimio manane, likiwamo la kuwawajibisha Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka.
Wengine waliowajibishwa pamoja na mawaziri hao ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema, na wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Umeme Nchini (Tanesco) na kuwavua nyazifa zao wenyeviti watatu wa kamati za kudumu za Bunge.
Wenyeviti waliovuliwa nyadhifa zao ni Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Victor Mwambalaswa, Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala, William Ngeleja na Kamati ya Bajeti, Andrew Chenge. Viongozi hao wamevuliwa nyadhifa zao chini ya azimio la Bunge namba mbili.
Maazimio hayo mapya manane yalisomwa bungeni jana jioni na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe.
Akizungumza bungeni Zitto alisema, mabilioni ya fedha yaliyotolewa kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow yametumika kuwapa kile kinachoonekana kuwa ni rushwa.
Zitto alisema baadhi ya watu waliochukua fedha hizo ni viongozi wa umma na maofisa wa Serikali kama mawaziri, majaji, wabunge, wenyeviti wa kamati za Bunge, wakuu wa taasisi za umma, viongozi wa dini, mawakili wa kujitegemea na watu binafsi.
“Vitendo vilivyofanywa na watu hawa vinaashiria uzembe na makosa mbalimbali ya jinai kama vile wizi, ubadhilifu kutakatisha fedha haramu, matumizi mabaya ya madaraka, rushwa na kupokea mali ya wizi,” alisema.
Alitaja azimio la kwanza la Bunge ni kulitaka Jeshi la Polisi na vyombo vingine husika vya ulinzi na usalama vichukue hatua stahiki kwa mujibu wa sheria za nchi yetu.
Zitto alisema watu wote waliotajwa na taarifa maalumu ya kamati kuhusika na vitendo vyote vya kijinai kuhusiana na miamala ya Akaunti ya Escrow na watu wengine watakaogundulika kufuatia uchunguzi mbalimbali unaoendelea kuhusika katika vitendo hivyo vya jinai, watachukuliwa hatua stahiki kwa mujibu wa sheria.
Azimio la tatu ni kuzitaka Kamati husika za kudumu za Bunge zichukue hatua za haraka na kwa vyovyote vile kabla ya mkutano wa 18 wa Bunge kuwavua nyazifa zao za wenyeviti wa kamati husika za Bunge. Zitto alitaja azimio la nne ni la kumuomba Rais auende Tume ya kijaji kuchunguza tuhuma za utovu wa maadili dhidi ya Jaji Aloysius Mujulizi na Jaji Profesa Eudes Ruhangisa wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Alisema utaratibu wa kushughulikia nidhamu za majaji kwa mujibu wa Katiba unamtaka Rais kuunda Tume ya Uchunguzi ya Kijaji, kuchunguza tuhuma za utovu wa maadili dhidi ya majaji.
Pia azimio la tano ni mamlaka husika za kifedha na za kiuchunguzi kuitaja Benki ya Stanbic na benki nyingine yoyote itakayogundulika kufuatia uchunguzi wa mamlaka za kiuchunguzi, kujihusisha na utakatishaji wa fedha zilizotolewa katika Akaunti ya Escrow, kuwa taasisi zenye shaka ya utakatishaji wa fedha haramu.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao