Kivumbi Uchaguzi Serikali za Mitaa

Dar es Salaam.
 Watanzania leo wanaingia kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji uliofunikwa na malalamiko kadhaa ya ukiukwaji wa kanuni, huku chama tawala CCM na wapinzani wakitambiana kushinda.
Tangu ulipotangazwa rasmi Septemba mwaka huu hadi jana, Jumamosi ambayo ilikuwa siku ya kufunga kampeni, mchakato wa uchaguzi huo umegubikwa na mapingamizi na dosari lukuki, mambo ambayo vyama vya siasa vya upinzani vinadai yataufanya usiwe huru na haki.
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), ukiongozwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), vinatuhumu kuwepo kwa faulo na uvunjaji mkubwa wa kununi uliofanywa na Serikali ili kukipa ushindi wa bure chama tawala, CCM.
Wagombea waenguliwa
Uchaguzi huo unafanyika leo, huku kukiwa tayari na wagombea 228 wa Chadema ambao wameenguliwa katika nafasi mbalimbali walizokuwa wakigombea kutokana na sababu tafauti.
Hadi kufikia Ijumaa iliyopita, kulikuwa na mapingamizi 257, ambayo hayajatolewa uamuzi jambo ambalo limewaacha baadhi ya wagombea katika giza nene la kutokujua hatma yao.
Tatizo la wingi wa mapingamizi na dosari nyingine ziliilazimu Chadema kumwandikia barua Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa nyakati tofauti ili aweze kuchukua hatua zaidi.
Desemba Mosi mwaka huu, Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe aliainisha kasoro kadhaa za uchaguzi huo ikiwamo sehemu A ya maelezo ya mgombea katika kipengele cha jinsi baadhi ya wagombea walioondolewa kutokana na kuandika kwa maneno, badala ya kukata maneno yaliyopo kwenye mabano ya me/ke.
Barua nyingine ya chama hicho kwa Pinda, iliandikwa na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa Novemba 14 mwaka huu. Katika barua hiyo Slaa alielezea baadhi ya dosari zilizopo katika Mwongozo wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na kuitaka Ofisi ya Waziri Mkuu kuzifanyia kazi.
Majibu ya Serikali
Mratibu wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kutoka Tamisemi, Denis Bandisa alisema kuwa wana taarifa ya mapingamizi mbalimbali katika mchakato wa uchaguzi huo, lakini mengi yameshughulikiwa na Kamati za Rufaa za Wilaya.
Bandisa aliwataka baadhi ya wagombea ambao hawakuridhika na uamuzi wa kamati hizo kwenda mahakamani kwa hatua zaidi, hasa baada ya Serikali kuwa tayari imetoa mwongozo wa taratibu wa rufaa.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao