Mwelekeo mpya; Ukawa wasema serikali ya mseto inanukia 2015

Dar es Salaam.
 Matokeo ya awali ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika nchi kote hivi karibuni yanaonyesha kuwa wananchi wamebadilisha mitazamo yao dhidi ya vyama vya siasa na hivyo kutoa picha mpya kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka 2015.
Uchaguzi huo uligubikwa na malalamiko katika baadhi ya maeneo nchini kiasi cha Serikali kuwaondoa kazini wakurugenzi wa halmashauri tano kwa kushindwa kuusimamia vyema, pia umevipa vyama na Serikali nafasi ya kujitafakari upya.
Kwa upande mmoja, uchaguzi huo umewapa nguvu wapinzani kwa kuongeza idadi ya viti, lakini umeivuta nyuma CCM baada ya kupoteza zaidi ya nafasi 2,600 za uenyekiti wa vijiji na mitaa ikilinganishwa na uchaguzi wa mwaka 2009 ilipopata jumla ya viti 12, 042.
Vyama vya upinzani vimefanikiwa kuongeza kibindoni viti 1,981 ikilinganishwa na uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika mwaka 2009 ambapo vilipata nafasi 1,230 za wenyeviti wa mitaa na vijiji.
Matokeo haya yametoa mwelekeo mpya kwa vyama vya siasa nchini, wapinzani wakiamini huo ndiyo ufunguo wao kuelekea Ikulu mwakani, CCM wakiamini kuwa huko ni kujikwaa tu na wataendelea kubaki Ikulu mwakani kwani bado wanakubalika kwa kiasi kikubwa.
Akizungumza mjini Dodoma hivi karibuni, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa (Tamisemi), Khalist Luanda alisema kwamba wakati CCM ikifanikiwa kupata ushindi wa jumla wa mitaa na vijiji 9,406, vyama vya upinzani vimepata nafasi 3,211.
Katika matokeo hayo CCM kimepata vijiji 7,290 kikifuatiwa na Chadema yenye vijiji 1,248. CUF imeshika nafasi ya tatu kwa kuwa na vijiji 946, ikifuatiwa na UDP yenye vijiji vinne na TLP na NLD vyenye viwili kila kimoja.
Katika nafasi za wenyeviti wa mtaa, CCM kimechukua jumla ya mitaa 2,116. vyama vingine na nafasi zao kwenye mabano ni Chadema (753), CUF (235), ACT (9), NCCR - Mageuzi (8) wakati vyama vya TLP, UMD, UDP na NRA vimepata mtaa mmoja kila kimoja.
Hata hivyo, katika baadhi ya maeneo nchini, wananchi watapiga kura leo baada ya kushindwa kufanya hivyo Desemba 14 kutokana na kasoro kadhaa zilizojitokeza.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia alisema matokeo hayo ni dalili kuwa CCM itafanya vizuri zaidi kwenye Uchaguzi Mkuu mwakani.
Ingawa waziri huyo alikiri kuwa vyama vya upinzani vimechukua maeneo mengi kuliko uchaguzi uliopita, alisema vyombo vya habari vinatumika kupotosha hali halisi na kuifanya CCM kuonekana kuwa imepoteza viti vingi kuliko uhalisia.
Matokeo hayo yanaonyesha CCM imepoteza viti zaidi katika mikoa wa Dodoma, Lindi, Mtwara, Iringa, Arusha, Singida na katika baadhi ya majimbo ya Dar es Salaam.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Matumizi ya simu kwa wanafunzi chanzo mmomonyoko wa maadili’

HATARI: Wengi wanunua sabuni za dawa bila maelekezo ya wataalamu

Wazazi timizeni wajibu wenu katika Malezi ili Watoto wenu wafikie Ndoto zao